Amunike keshawaondoa kina Ajib, muhimu wafanyie kazi mapungufu


Ukizungumzia wachezaji walion'gara ligi kuu ya Tanzania Bara msimu uliomalizika, huwezi kukosa kutaja jina la Ibrahim Ajib, kiungo wa Yanga ambaye aliibuka kinara wa kutengeneza nafasi za mabao

Ajib alihusika katika karibu nusu ya mabao ya Yanga akitoa pasi za mabao 17 na mwenyewe kufunga mabao sita

Hata hivyo takwimu hizo hazikumsaidia kupata nafasi ya kushiriki michuano ya AFCON 2019, michuano ambayo kila mchezaji barani Afrika angependa kushiriki

Ajib ni miongoni mwa wachezaji saba walioenguliwa hatua ya awali kabisa na kocha Emmanuel Amunike

Aliiondolewa katika kikosi cha wachezaji 32 waliosafiri kwenda Misri jana

Wachezaji wengine walioenguliwa ni Jonas Mkude, Ayoub Lyanga, Ally Khamis, Kenned Wilson, Ally Ally na Shomari Kapombe

Sababu iliyotolewa na Amunike ambayo ilipelekea wachezaji hao kuenguliwa ni suala la nidhamu na 'performance' yao mazoezini

Licha ya wadau wengi kutokubaliana na hatua ya kuwaengua nyota hao hasa Ajib na Mkude, bado uamuzi wa kocha unabaki kuwa wa mwisho na hakuna namna zaidi ya kuuheshimu

Lakini uamuzi huo hauondoi ubora wa wachezaji hao, muhimu wanapaswa kuyafanyia kazi mapungufu yaliyoainishwa (kama yapo)

Nakumbuka kuna wakati kocha wa Yanga Mwinyi Zahera alimkosoa sana Ajib waziwazi akimtaka aongeze juhudi mazoezini ili awe bora zaidi

Zahera alisema Ajib ni mchezaji mwenye kipaji miongoni mwa wachezaji aliowashuhudia hapa Tanzania lakini akasisitiza anapaswa kujitambua na kuhakikisha anadhihirisha ubora wake

Mara kwa mara Ajib alilaumiwa kwa kukosa mazoezi/mechi kutokana sababu nyepesi

Michezo mitano ya mwisho ya Yanga kumaliza msimu Ajib hakuonekana dimbani sababu ikilelezwa alikuwa mgonjwa

Wasichofahamu wachezaji ni kuwa wanapoitwa kwenye timu za Taifa, taarifa zao katika timu wanazocheza huwa zinaambatanishwa

Sasa inapotokea taarifa zako zinakuwa na 'walakini' inaweza kuwa sababu ya kocha 'kukuwekea zengwe' hasa ikiwa yeye binafsi hakukubali


from sokoa news http://bit.ly/2QYyZNK
1

Post a Comment

0 Comments