Ajib mtegoni Yanga


Inaelezwa nahodha wa Yanga Ibrahim Ajib tayari alishasaini mkataba wa awali kunako timu yake ya zamani ya Simba

Hata hivyo kinara huyo wa pasi za mabao msimu uliomalizika anaweza 'kubadili gia angani' kuendelea kubaki Jangwani, imefahamika

Hivi karibuni Makamu Mwenyekiti wa Yanga Fredrick Mwakalebela alisema kuwa Ajib yuko kwenye mipango ya kocha Mwinyi Zahera kwa ajili ya msimu ujao

Kilichokuwa kinasubiliwa ni yeye kufanya uamuzi ili apewe mkataba mpya

Baada ya dili la kiungo huyo kutimkia TP Mazembe kushindikana, Mwakalebela alimtaka asaini mkataba mpya Yanga

"Tunamwambia Ajib hana sababu ya kwenda kokote, abaki nyumbani kwani kumenoga!," alisema Mwakalebela

Ishu ya kujiunga na Simba

Inaelezwa kuna mvutano baina ya mabosi wa Simba juu ya usajili wa Ajib kutokana na timu hiyo kuwa na wachezaji wengi kwenye nafasi anayocheza

Simba inadaiwa kuwa mbioni kumsajili kiungo wa Gor Mahia Francis Kahata, usajili ambao kama utakamilika, utaondoa kabisa sababu ya Ajib kusajiliwa

Aidha hata kama atasajiliwa na Simba, Ajib atakuwa na nafasi finyu ya kucheza kwenye kikosi cha kwanza kwa kuwa hakupendekezwa na kocha wa timu hiyo Patrick Aussems

Inaelezwa Mo ndiye anayetaka Ajib arudi Simba

Ushiriki ligi ya mabingwa wampa mzuka

Baada ya Yanga kupata nafasi ya kushiriki michuano ya ligi ya mabingwa msimu ujao, inaweza kuwa sababu ya fundi huyo wa mpira kubaki Jangwani

Wengi wanaamini Ajib atafanikiwa zaidi akicheza Yanga kuliko Simba

Tayari ameweza kumshawishi kocha Mwinyi Zahera, hivyo akiendelea kubaki atakuwa na nafasi nzuri zaidi ya kuendelea kun'gara

Baadhi ya wachezaji wapya waliosajiliwa na Yanga wameonyesha shauku ya kutaka kucheza pamoja na kiungo huyo aliyetengeneza mabao 17 na kufunga mabao sita msimu uliomalizika

Winga Issa Birigimana aliyesajiliwa na Yanga kutoka APR amewataja Ibrahim Ajib na Papi Tshishimbi kuwa wachezaji wanaomvutia sana na atafurahi kucheza nao kikosini

Hata hivyo uongozi wa Yanga hauonekani kuwa na presha ya kutaka kumsajili Ajib

Wamemtaka mwenyewe kuamua kama anakubali kubaki kwa ofa aliyowekewa mezani au kufuata mamilioni ya Mo Msimbazi

Baada ya kuenguliwa kwenye timu ya Taifa na kocha Emmanuel Amunike, Ajib anaendekea kujifua mchangani kujiandaa na changamoto za msimu ujao


from sokoa news http://bit.ly/2ZeqKzJ
1

Post a Comment

0 Comments